Yanga 'meno nje' ikiishusha Simba SC Ligi Kuu

© Kwa Hisani

KANDANDA Yanga 'meno nje' ikiishusha Simba SC Ligi Kuu

Zahoro Mlanzi • 07:45 - 08.10.2023

Ushindi huo, umeifanya Yanga kujikusanyia alama 12 na kushika nafasi ya pili katika msimamo wa ligi sawa na Simba SC iliyo nafasi ya tatu.

Timu ya Yanga SC, imerejea katika muendelezo wake wa ushindi baada ya kuifunga Geita Gold FC mabao 3-0, mchezo uliopigwa Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Mabingwa hao wa kihistoria wa ligi hiyo, waliingia katika mchezo huo wakitoka kufungwa mabao 2-1 na Ihefu FC kitu ambacho kilizua gumzo mitaani.

Ushindi huo, umeifanya Yanga kujikusanyia alama 12 na kushika nafasi ya pili katika msimamo wa ligi sawa na Simba SC iliyo nafasi ya tatu ambayo kesho itacheza na Singida Fountain Gate ugenini mkoani Singida.

Nafasi ya kwanza katika ligi hiyo inashikiliwa na Azam FC ambayo jana iliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Coastal na kufikisha alama 13.

Mabao ya Yanga, yamefungwa na Pacome Zoazoua, Stephen Aziz KI na Max Nzengeli ambapo kila mmoja sasa amefikisha mabao matatu kwenye ligi hiyo.

Geita ambayo imebaki na alama 4 ikishika nafasi ya 12, kipindi cha kwanza imecheza kwa kujilinda sana kitu kilichoifanya Yanga kutawala mchezo na kuliandama lango la Geita kwa mashambilizi mfululizo.

Timu hizo hadi zinakwenda mapumziko, Yanga imekuwa mbele kwa mabao 2-0 yaliyofungwa na Pacome na Azizi KI.

Hata hivyo, Geita haikupiga shuti hata moja lililolenga goli zaidi ya kupata pigo baada ya straika wao, Elius Maguli kuumia na kuingia Valentino Mashaka.

Kipindi cha pili, Geita imeamua kufunguka na kujikuta nusura ifunge bao dakika ya 53 kupitia kwa Valentino ambaye akiwa nje ya eneo la hatari alipiga shuti lilitoka sentimeta chache langoni mwa Yanga.

Pamoja na kupambana kutaka kusawazisha, Geita ilijikuta na mlima mrefu zaidi baada ya kufungwa bao la tatu dakika ya 68 na Nzengeli aliyeunasa mpira ulioporwa na Mudathir Yahya kutoka katika miguu ya Samuel Onditi na kupiga shuti lililojaa moja kwa moja wavuni huku Kipa, Sebusebu Samson akiruka bila mafanikio.

Katika mchezo mwingine uliopigwa muda mmoja na huo, wenyeji KMC FC, imeibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Ihefu FC, mchezo uliopigwa Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Bao pekee la KMC limefungwa na Ibrahim Elius na kunifanya timu hiyo kupanda hadi nafasi ya nne katika msimamo wa ligi hiyo nyuma ya Simba kwa alama zao 10.