Simba SC yalamba dili la shilingi bilioni 1.5 kwa muda wa miaka mitatu

Ligi Kuu Simba SC yalamba dili la shilingi bilioni 1.5 kwa muda wa miaka mitatu

Zahoro Mlanzi • 13:15 - 01.11.2023

Makubaliano hayo udhamini yatakuwa na faida kwa pande zote

Klabu ya Simba SC, imeingia mkataba wa miaka mitatu na Kampuni ya Serengeti Breweries kupitia bia yake ya Pilsner Lager.

Akizungumza Mtendaji Mkuu wa klabu hiyo, Imani Kajula amesema udhamini huo umekuja kuongeza kitu kikubwa sababu uendeshaji wa timu unagharimu kiasi kikubwa cha fedha.

Kajula amesema makubaliano hayo yatakuwa na faida kwa pande zote huku aliwahakikishia Pilsner kurejea kwa kishindo kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.

“Tunawashukuru Serengeti kwa udhamini huu, hamjakosea kutuamiani, mmekuja kwenye klabu sahihi. Tunaamini muungano huu utakuwa na manufaa makubwa kwa pande zote mbili,” amesema Kajula.

Kwa upande wa Mkurugenzi Mkuu wa Serengeti Breweries, Obina Anyarebenchi, amesema makubaliano ya leo lengo lake sio tu kukuza chapa ya Pilsner bali ni kuhakikisha Watanzania wanafurahia.

“Serengeti tunajivunia mkataba huu, hatujakuja Simba kwa bahati mbaya bali tunaujua ukubwa wa Simba na tunaamini utakuwa na faida kwetu pamoja na wenzetu,” amesema Obina.

Akitoa neno la shukurani kwa niaba ya Bodi ya Wakurugenzi wa klabu hiyo, Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa klabu hiyo, Raphael Chegeni, amesema Serengeti imewekeza sehemu sahihi na matunda yake wataanza kuyaona kuanzia sasa.

“Karibuni na mmekuja sehemu sahihi wenye furaha. Simba ni timu kubwa na kwakuanzia Jumapili mtaanza kupata furaha,” amesema Chegeni.

Simba kwa sasa ipo kambini kujiandaa na mechi yao dhidi ya Yanga itakayopigwa Jumapili Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

Timu hizo zitaingia katika mchezo huo zikiwa na alama sawa 18 ila zinatofautiana kwa mabao na kuifanya Yanga kuwa kinara kwenye ligi hiyo.

Tufuatilie kwenye mtandao wetu wa kijamii wa WhatsApp ili uweze kupata habari zaidi kuhusu spoti.

Tags: