Simba SC kutimua wachezaji wavivu, wasiojituma

KANDANDA Simba SC kutimua wachezaji wavivu, wasiojituma

Na Zahoro Mlanzi • 22:00 - 15.11.2023

Tumekubaliana kutoendelea kufanya kazi kwa mazoea na kwamba tutachukuwa hatua stahiki ili kuboresha kikosi chetu hasa katika usajili unaokuja wa Januari

Wakati dirisha dogo la usajili kwa timu za Tanzania likitarajiwa kufunguliwa Desemba 15, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Klabu ya Simba, Salim Abdallah 'Try Again', amesema watalitumia dirisha hilo kuwaondoa wachezaji wote wavivu na wasiojituma.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Try Again amesema kama uongozi wamejipanga kupitisha panga na hivyo wanawataka wachezaji wote ambao wanataka kusalia klabuni hapo waoneshe kwa vitendo uwanjani.

"Tumekubaliana kutoendelea kufanya kazi kwa mazoea na kwamba tutachukuwa hatua stahiki ili kuboresha kikosi chetu hasa katika usajili unaokuja wa Januari," amesema.

Simba kwasasa wapo katika mchakato wa kutafuta kocha mpya ambaye anatarajiwa kutangazwa muda wowote kwa ajili ya kuziba pengo lililoachwa Kocha Roberto Oliveira 'Robertinho'.

Kwa mujibu wa taarifa za ndani za klabu hiyo, kocha mpya ameshapatikana na kwamba kinachosubiriwa ni siku tu ya kumtangaza.

Katika msimamo wa Ligi Kuu Bara, Simba inashika nafasi ya tatu ikiwa na alama 19 sawa na Azam FC huku Yanga ikiongoza kwa alama 24.

Katika hatua nyingine, Rais wa Heshima wa klabu hiyo, Mohamed Dewji 'Mo Dewji', amewataka wana-Simba kutulia na kuwa na imani na viongozi wao waliopo madarakani.

"Wana Simba tulieni, tuwaamini viongozi wetu," amesema kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram.

Kauli hiyo imekuja baada ya kuwepo kwa mvutano kwa baadhi ya wanachama wanaoshinikiza uongozi wa juu wa timu hiyo kujiuzulu kutokana na kichapo cha mabao 5-1 kutoka kwa Yanga.

Tangu Simba ifungwe mabao hayo, Mo Dewji hakusikika akizungumza chchote hadi alipoamua kuandika ujumbe huo.

Tags: