Kocha wa Simba SC Roberto Oliviera ataka klabu yake iogopwe Afrika

Kocha wa Simba SC Roberto Oliviera ataka klabu yake iogopwe Afrika

Zahoro Mlanzi • 18:00 - 25.10.2023

Alisema maneno hayo baada ya kulazimisha sare ya bao 1-1 dhidi ya Al Ahly kwenye uwanja wa ugenini na kutupwa nje ya michuano ya AFL.

Kocha wa Klabu ya soka ya Simba, Roberto Oliviera 'Robertinho', amesema umefika wakati sasa kwa timu barani Afrika kuanza kuogopa kucheza na timu yake.

Hayo ameyasema mara baada ya kulazimisha sare ya bao 1-1 dhidi ya Al Ahly kwenye uwanja wa ugenini na kutupwa nje ya michuano ya AFL.

Simba wameondoshwa kwenye michuano hiyo kwa kanuni ya bao la ugenini baada ya kutoka sare ya mabao 2-2 kwenye mchezo wa kwanza, hivyo kufanya matokeo ya jumla kuwa 3-3 na Ahly kunufaika na bao la ugenini.

Akizungumza na Pulsesports baada ya kutua salama jijini Dar es Salaam wakitokea Misri, Robertinho amesema mechi ilikuwa ngumu lakini timu yake ilitoa upinzani mkali kitu ambacho kinapaswa kuwa fundisho kwa timu nyingine zinazopangwa kucheza na Simba.

"Tulitarajia mchezo mgumu hasa tukiwa ugenini na kweli mechi ilikuwa ngumu, hata hivyo wachezaji wangu walihimili presha ya mchezo na tukapambana vizuri dhidi ya Al Ahly timu ambayo ina kila sifa nzuri barani Afrika," alisema.

Kocha huyo raia wa Brazil hakusita kuwamwagia sifa wachezaji wake kwa kuonesha ukomavu na kwamba amekiri kuna hatua kubwa wamepiga kama klabu na nchi kwa ujumla.

Robertinho ametaja mbinu ambazo alizitumia kwenye mchezo huo, kuwa aliwaagiza wachezaji wake wawe wengi na wasiache nafasi kwa adui mbele ya lango lao na hiyo mbinu ndo iliwapa wakati mgumu Al Ahly.

Hii inakuwa ni mara ya kwanza kwa Simba kupata sare dhidi ya Al Ahly ugenini kwenye michuano ya klabu barani Afrika.

Tags: