Azizi Ki, Robertinho watwaa Tuzo ya Oktoba

Ligi Kuu Azizi Ki, Robertinho watwaa Tuzo ya Oktoba

Na Zahoro Mlanzi • 09:35 - 04.11.2023

Hiyo inakuwa ni tuzo ya pili kwa Azizi Ki ndani ya wiki hii ambapo hivi karibuni alishinda tuzo ya mchezaji bora ndani ya Yanga.

Kiungo mshambuliaji wa timu ya Yanga, Stephane Aziz Ki, ameshinda tuzo ya Mchezaji Bora wa Oktoba ya Ligi Kuu Tanzania Bara.

Aziz Ki amewashinda Max Nzengeli ambaye anacheza naye kwenye Yanga na Moses Phiri wa Simba.

Katika mwezi huo, Ki alicheza dakika 278 sawa na mechi 4 ambapo alifunga mabao manne.

Hii inakuwa ni tuzo ya pili kwa Ki ndani ya wiki hii ambapo mapema alishinda tuzo ya mchezaji bora ndani ya Yanga.

Wakati huo huo, Kocha wa Simba, Roberto Oliveira 'Robertinho', ameshinda tuzo ya Kocha Bora akiwashinda Miguel Gamondi wa Yanga na Abdulhamid Moalin wa Coastal Union.

Katika mwezi huo, Robertinho ameiongoza Simba kwenye mechi tatu ambazo wameshinda zote dhidi ya Tanzania Prisons, Singida FG na Ihefu.

Pia Meneja wa Uwanja wa Highland Estate, Malule Omar ameshinda tuzo ya Meneja Bora wa uwanja.

Uwanja huo ambao upo wilaya ya Mbarari mkoani Mbeya, unamilikiwa na klabu ya soka ya Ihefu.